Friday, May 21, 2010

SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA CCM WILAYANI KYELA!!!

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Mkoa wa Mbeya, Bwana Nawab Mullah kutokana na kifo cha Mwenyekiti wa CCM wa Wilaya ya Kyela, Marehemu Japhet Mwakasumi, aliyefariki tarehe 19 Mei, 2010 Jijini Dar es Salaam.

Katika salamu zake hizo, Rais Jakaya Kikwete amesema amesikitishwa na kuhuzunishwa sana na taarifa za kifo cha Marehemu Mwakasumi kilichotokea nyumbani kwake Ukonga – Banana, Jijini Dar es Salaam.

“Ninatambua vema mchango wa Marehemu Mwakasumi wakati wa uhai wake katika Wilaya ya Kyela hususan katika Chama Cha Mapinduzi kutokana na uhodari na uchapakazi wake ambao umeiwezesha CCM kuimarika zaidi, “amesema Rais Kikwete na kuongeza, “Kwa hakika kifo chake ni pigo kubwa kwa familia yake, wana – CCM na wananchi wote wa Wilaya ya Kyela, Mkoa wa Mbeya na Taifa kwa ujumla”

Katika rambirambi zake kwa familia ya Marehemu Japhet Mwakasumi, Rais Kikwete amesema familia hiyo imepoteza kiongozi muhimu. Amewataka ndugu, jamaa na marafiki wa Marehemu Mwakasumi kuwa na moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo, na amemuomba Mwenyezi Mungu ailaze mahali pema peponi roho ya Marehemu Japhet Mwakasumi.

No comments:

Post a Comment