Tuesday, January 3, 2012

RATIBA YA SHEREHE ZA MAPINDUZI YA ZANZIBAR YATOLEWA!!

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imetoa ratiba ya sherehe za kuadhimisha miaka 48 ya Mapinduzi ya Zanzibar ambazo zinaanza rasmi kesho katika majimbo yote 50 ya Unguja na Pemba

Katibu wa Kamati ya Sherehe hizo Dk. Khalid Mohamed amesema kuanzia kesho kutakuwa na kazi ya usafishaji mazingira katika majimbo yote 50 ya Zanzibar ambapo wasimamizi wa zoezi hilo ni Halimashauri za Wilaya, Baraza la Manispaa,Mabaraza ya Miji na Masheha.

Kwa mujibu wa Ratiba hiyo inaonesha kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohammed Shein atazindua Jengo la Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) huko Mazizini Mkoa wa Mjini Magharibi

Aidha Rais Shein anatarajiwa pia kuzindua Barabara ya Dunga-Amani katika hafala itakayofanyika huko Dunga Mkoa wa Kusini Unguja ambapo Januari 9 atafungua barabara mbili (2) za Wilaya ya Chake Chake Pemba ambazo ni Chanjamjawiri-Tundaua na Chanjamjawiri-Pujini.

Katika hatua nyingine Rais Shein anatarajiwa kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Nyumba ya Madaktari kutoka Norway katika Chuo cha Afya cha Mbweni Mkoa wa Mjini Magharibi

Halikakadhalika Rais Shein atafungua Barabara nne (4) za Wilaya ya Mkoani Kisiwani Pemba ikiwemo Mtambile-Kengeja, Mtambile-Kangani, Mizingani-Wambaa na Kenya-Chambani

Shughuli nyengine atakazofanya Dk.Shein ni Ufunguzi wa Jengo la Ofisi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi huko Weni Mkoa wa Kaskazini Pemba na ataendesha zoezi la kuchangia Mfuko wa Fedha za Mikopo (Fund Rising) katika Hoteli ya Bwawani Mjini Zanzibar

Wakati huo huo Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim seif Sharif Hamad anatarajiwa kuzindua Jengo la Ofisi ya Makao Makuu ya Mfuko wa Barabara Zanzibar ambapo jioni yake atafungua Jengo la Idara ya Uvuvi liliopo Maruhubi katika Mkoa wa Mjini Magharibi

Aidha Maalim seif Sharif Hamad atafungua Tangi la Maji Gongoni Wilaya ya Micheweni Pemba ikiwa ni shamra sharma za kutimiza mika 48 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Naye Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika hafla ya Ufunguzi wa Skuli ya Mkanyageni Mkoa wa Kusini Pemba ambapo pia atafungua Soko la Jumapili (Sunday Market) kwa wajasiriamali liliopo Michenzani Mkoa wa Mjini Magharibi

Viongozi wengine watakaofungua miradi mbalimbali ya maendeleo kwa nyakati tofauti ni pamoja na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Mohamed Gharib Bilal Mke wa Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania Mama Salma Kikwete na Marais Wastaafu wa Zanzibar

Wengine ni pamoja na Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao watahusika na ufunguzi wa miradi mbali mbali ya maedeleo

Shamra sharma za Sherehe za kutimiza miaka 48 ya Mapinduzi Zanzibar zimenza jana na ziaendelea katika mikoa yote ya Zanzibar ambapo kilele chake kitafikiwa Januari 12 katika kiwanja cha Aman Mjini Zanibar

No comments:

Post a Comment