Thursday, December 29, 2011

RAIS KIKWETE ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KWA KIFO CHA HALIMA MCHUKA!!

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Bwana Clement Mshana, kuomboleza kifo cha mtangazaji maarufu wa shirika hilo, Bi Halima Mohammed Mchuka ambaye alifariki dunia usiku wa kuamkia leo, Alhamisi, Desemba 29, 2011 kwenye Hospitali ya Taifa Muhimbili, Dar es Salaam.

“Nimepokea kwa huzuni habari za kifo cha Halima Mohammed Mchuka. Nakutumia wewe Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) salamu za dhati ya moyo wangu kuomboleza kifo chake. Nakuomba, kupitia kwako, uniwasilishie salamu zangu kwa wafanyakazi wenzake katika TBC ambao wamempoteza mwenzao na rafiki yao.”

Ameongeza Mheshimiwa Rais katika salamu zake, “Aidha, nataka kupitia kwako niwatumie salamu zangu za rambirambi wana-familia, ndugu na jamaa wote za marehemu. Wajulishe kuwa niko nao katika wakati huu wa maombolezo na kwamba msiba wao ni msiba wangu pia. Nawaomba wawe na moyo wa subira katika kipindi hiki kigumu kwa sababu yote ni mapenzi ya Mungu. Naungana nao kumwomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, ailaze pema peponi roho ya marehemu. Amen.”

Mheshimiwa Rais pia amesema kuwa Bi. Mchuka ametoa mchango mkubwa katika nyanja ya utangazaji nchini. “Sote tutaendelea kukumbuka weledi wake, uzalendo wake na ujasiri wake katika utangazaji uliomsukuma kuwa Mwanamke wa Kwanza katika Tanzania kutangaza mechi za mpira wa miguu”.

Ameongeza Rais Kikwete: “Ni dhahiri kuwa nyanja ya utangazaji imeondokewa na mtu muhimu na namna nzuri zaidi ya kumuenzi Bi. Mchuka ni kwa watangazaji waliobakia kuendelea kuiga mfano wake katika ubora wa utangazaji nchini mwetu.”

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
29 Desemba, 2011

No comments:

Post a Comment