Wednesday, April 6, 2011

RWEGASIRA WA TRAWU KUZIKWA LEO IKULU YATUMA RAMBIRAMBI!!

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Waziri wa Uchukuzi, Mheshimiwa Omar Nundu kufuatia kifo cha ghafla cha Sylvester Rwegasira, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Wafanyakazi wa Reli Tanzania (TRAWU) kilichotokea tarehe 4 Aprili, 2011 kutokana na maradhi ya moyo.

Rais Kikwete amesema kuwa kifo cha Sylvester Rwegasira kimeleta simanzi kubwa siyo kwa familia yake tu, bali pia jumuiya ya wafanyakazi hapa nchini kwani Marehemu Sylvester alikuwa mtetezi mkubwa wa wafanyakazi hususan wale wa Reli ambao yeye alikuwa Katibu Mkuu wa Chama chao, kwani alijitoa kwa moyo wake wote kutetea maslahi yao.

Kupitia kwa Waziri wa Uchukuzi, Rais Kikwete ametoa pole nyingi kwa familia ya Marehemu Sylvester Rwegasira kwa kupotelewa na kiongozi muhimu wa familia, hivyo anamuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aiweke mahali pema peponi roho ya Marehemu Rwegasira.

Wakati huo huo, Rais Kikwete amewaomba wanafamilia ya Marehemu Rwegasira kuwa watulivu, wavumilivu na wenye subira katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo ya mpendwa wao, huku akiwahakikishia kuwa yeye binafsi yuko pamoja nao katika muda wote wa maombolezo ya Marehemu Sylvester Rwegasira.

No comments:

Post a Comment