Thursday, April 21, 2011

RAIS KIKWETE AKUTANA NA VIONGOZI WA WAFANYAKAZI IKULU!!

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete Jumatano, Aprili 20, 2011, amekutana na kufanya mazungumzo na viongozi wa vyama vya wafanyakazi nchini.

Mkutano huo wa kawaida kati ya Rais Kikwete na vikundi mbalimbali vya jamii kikiwemo kile cha viongozi wa wafanyakazi umefanyika Ikulu, Dar es Salaam katika mazingira ya kuelewana.

Mkutano huo umechukua kiasi cha saa tano na kuhudhuriwa na viongozi 20 wa wafanyakazi, mawaziri wanaohusika na masuala na haki za wafanyakazi na watumishi wengine waandamizi wa Serikali.

Viongozi wao wakiongozwa na Rais wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Bwana Ayoub Omar Jumaa umeshirikisha viongozi kutoka TUCTA yenyewe, Chama cha Walimu Tanzania (CWT), TPWU, TEWUTA, DOWUTA, TRAWU, CHODAWU, TUICO, TASU, TAMICO TUGHE na COTWU.

Mawaziri waliohudhuria mkutano huo ni pamoja na Waziri wa Kazi na Ajira, Mheshimiwa Gaudencia M. Kabaka, Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi Umma, Mheshimiwa Hawa A. Ghasia na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) Mheshimiwa George Huruma Mkuchika.

Katika kikao hicho, pande hizo mbili zimejadili masuala mengi yanayohusu haki na maslahi ya wafanyakazi na masuala mengine muhimu ya taifa yakiwamo madai ya malimbikizo ya malipo ya wafanyakazi ikiwamo mishahara.

Rais Kikwete na viongozi hao pia wamejadili kuhusu uwezekano wa Serikali kuongeza mishahara ya watumishi kwa kuzingatia upandaji wa gharama za maisha, uwakilishi wa wafanyakazi katika mchakato wa kuandaa Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na uwezekano wa Serikali kupunguza kodi kwa wananchi ili kutoa ahueni zaidi ya maisha kwa wananchi.

Kuhusu sera ya Serikali ya kupunguza kodi ili kutoa ahueni ya maisha kwa wananchi, Rais Kikwete amewaambia viongozi hao wafanyakazi: “Hili tulikwishakubaliana kuwa lazima tuchukue hatua za mara kwa mara kuongeza unafuu wa maisha kwa wananchi wetu. Tutaendelea nalo hili kwa sababu ni muhimu sana. Suala kubwa hapa ni kutekeleza sera ya kupunguza ukali wa maisha kwa wananchi. Lazima tufanye kila liwezekanalo kufanikisha hili.”

Kuhusu ombi la viongozi hao kuwa Serikali itoe dhamana kwa Shirika la Simu Tanzania (TTCL) ili kuliwezesha shirika kuwa na uwezo wa kukopa fedha katika mabenki kusaidia kuliimarisha, Rais Kikwete ameigiza Wizara ya Fedha kuchukua hatua za haraka kuhakikisha hili linafanikiwa. “Tulifanye hili haraka sana, halina sababu ya kucheleweshwa kwa sababu TTCL ni shirika muhimu sana.”

No comments:

Post a Comment