Wednesday, May 4, 2011

RAIS KIKWETE KWENYE MKUTANO WA KIUCHUMI HUKO SAUZI!!

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete atakuwa mgeni maalum katika mjadala wa kimataifa kuhusu Visheni Mpya ya Kilimo katika Afrika (Achieving Africa’s New Vision for Agriculture) utakaofanyika mjini Cape Town, Afrika Kusini, Jumatano, Mei 4, 2011.

Rais Kikwete pia atatembelea Kituo cha Kimataifa cha Biashara (World Trade Centre) mjini humo humo kuona maandalizi yanayofanywa kwa ajili ya kuanzisha kituo kama hicho nchini Tanzania.

Aidha, kesho hiyo hiyo, Rais Kikwete atashiriki katika mjadala maalum wa maandalizi ya kuanzishwa kwa Soko la Mazao nchini (Commodity Exchange) ambalo maandalizi yake yanafanywa kwa pamoja kati ya Serikali ya Tanzania na Benki ya Dunia (WB).

Rais Kikwete atashiriki katika shughuli hizo muhimu kwa uchumi na maendeleo ya Tanzania ikiwa sehemu ya ushiriki wake katika Mkutano wa Uchumi Duniani – Kanda ya Afrika (World Economic Forum-Africa) unaofanyika mjini Cape Town, Afrika Kusini.

Mwaka jana, mkutano huo ulifanyika mjini Dar es Salaam, ikiwa ni mara ya kwanza kwa mkutano huo kufanyika nje ya mji wa Cape Town katika historia yake.

Rais Kikwete ameondoka nchini Jumanne, Mei 3, 2011, kwenda Cape Town kwa ajili ya mkutano huo wa siku mbili ambako pia atashiriki katika shughuli nyingine tatu kuhusu uchumi na maendeleo.

Washiriki wengine wa mkutano wa Visheni Mpya ya Kilimo katika Afrika, ambako Rais Kikwete atakuwa mgeni maalum, ni pamoja na viongozi mbalimbali duniani wa serikali, biashara na uchumi, mashirika ya kimataifa, mashirika yasiyokuwa ya kimataifa, wasomi na vyama vya wakulima duniani.

No comments:

Post a Comment